Social Icons

Sunday 18 March 2012

WASSIRA AMVAA DR WILBROD SLAA


Dk Slaa anatua Arumeru kipindi ambacho anasubiriwa kujibu tuhuma zilizotolewa na Wassira ambaye pia ni mlezi wa CCM mkoa wa Arusha.



Wassira katika mikutano mbalimbali ya kumnadi Sioi juzi na jana, alidai kwamba Dk Slaa anawajibika kuwajibu Watanzania sababu za kufukuzwa kwake ukasisi ndani ya Kanisa Katoliki, kabla ya kuingia kwenye siasa.



Wassira alisema Dk Slaa ambaye amekuwa msitari wa mbele kukemea ufisadi nchini, si mkweli kwani alifukuzwa baada ya kutafuna fedha za ujio wa Papa John Paul – II aliyezuru Tanzania mwaka 1990, wakati huo Slaa akiwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).



“Huyu Dk Slaa alitafuna fedha za ujio wa Papa miaka ya nyuma na ndio chanzo cha kufukuzwa upadri,tena haya hata nyie mlichanga hizo fedha kwenye vigango vya parokia si mnakumbuka,”alisema Wassira.



Wassira aliendelea kumtuhumu Dk Slaa kwamba anaendeleza ufisadi ndani ya Chadema kwa kile alichodai kwamba alimfukuza kazi mhasibu wa chama hicho, kwa kosa la kushindwa kumlipa mchumba wa Dk Slaa, Josephine Mushumbusi kiasi cha Sh10 milioni.



Wakati huo huo,Wassira ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alisema kwamba mgombea ubunge wa Chadema,Joshua Nassari hafai kuwa mbunge wa jimbo hilo kwa kuwa ni kijana mkorofi na mara kwa mara, baba yake mzazi amekuwa akimsihi kuachana na ukorofi tangu wakati akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.



Alisema kwamba baba wa mgombea huyo ambaye ni kiongozi wa dini, amekuwa akimsihi kuachana na ukorofi ikiwa ni pamoja na kuoa ili aweze kutulia lakini cha ajabu, Nassari amekuwa akionekana na bibi wa kizungu mwenye umri wa zaidi ya miaka 60 akizunguka naye mitaani jijini Arusha.



Wakati Wassira akitoa kauli hiyo, baba yake Nassari, Mchungaji Samuel Nassari na mkewe walihudhuria uzinduzi wa kampeni za mtoto wao zilizofanyika Jumamosi ya wiki jana kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Leganga, Usa River.



No comments:

LATEST NEWS

Share

Widgets

 

Total Pageviews